1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Samia apokea ripoti ya CAG, madudu yaanikwa wazi

Deo Kaji Makomba
28 Machi 2024

Mkaguzi wa Hesabu za Serikali nchini Tanzania Charles Kichere awasilisha ripoti ya ukaguzi inayoonyesha mashirika nane ya umma yalikusanya mapato ya shilingi bilioni 23.27 kinyume na utaratibu.

https://p.dw.com/p/4eERD
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan Machi 28. 03.2024 amepokea ripoti ya mkaguzi wa hesabu za serikali na kuwataka wahusika kuifanyia kazi Picha: Presidential Press Service Tanzania

Mdhibiti na Mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali CAG, nchini Tanzania Charles Kichere amewasilisha ripoti yake ya mwaka 2022/2023 kwa Rais Samia Suluhu Hassan ambayo imebainisha kuwa mashirika nane ya umma yalikusanya mapato ya shilingi bilioni 23.27 nje ya mfumo wa kielekroniki wa malipo ya serikali kinyume na utaratibu.

Akipokea ripoti hiyo ya awali ya Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali na taarifa ya utendaji kazi wa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa, TAKUKURU, Rais Samia amesema kuwa ripoti hizo zinazosomwa kila mwaka zinachangia maboresho au kuimarisha utendaji ndani ya serikali na mashirika ya umma.

Amesema "Sababu dosari zilizotolewa hapa, tutakwenda kukaa tuzifanyie kazi, turekebishe na mwakani pengine hizi hazitajirudia, na tutakuwa tumesogea." 

Soma pia:Tanzania: Majadala kuhusu ripoti ya CAG kufanyika bungeni Novemba

Daressalam nchini Tanzania
Shirika la simu nchini Tanzania, TTCL limetajwa kupata hasara kwenye ripoti ya CAG nchini TanzaniaPicha: ingimage/IMAGO

Awali akiwasilisha ripoti hiyo kwa Rais Samia Suluhu Hassan ikilu ya Chamwino jijini Dodoma mdhibiti na mkaguzi huyo wa hesabu za serikali Charles Kichere, amesema kuwa mashirika nane ya umma yalikusanya mapato ya shilingi bilioni 23.27 nje ya mfumo wa kielekroniki wa malipo ya serikali GPG kinyume na waraka wa hazina namba tatu 2017.

Amesema kushindwa kukusanya mapato kwa mfumo huo kunaweza kusababisha kufifisha juhudi za udhibiti wa mapato na uwazi katika mapato ya serikali.

Aidha mdhibiti na mkaguzi huyo wa hesabu za serikali ameongeza kusema kuwa, amebaini mashirika ya umma yanayojiendesha kibiashara yamepata hasara kwa mwaka wa fedha 2022/2023 ikiwemo Shirika la ndege nchini Tanzania ATCL licha ya hatua zinazochukuliwa na serikali kuhakikisha kuwa shirika hilo linajiendesha kwa faida.

Mashirika mengine ya umma yaliyopata hasara kwa mwaka wa fedha 2022/2023 ni Shirika la Mawasiliano TTCL ambalo limerikodi hasara ya shilingi milioni 894, licha ya kupokea ruzuku ya shilingi bilioni 4.55 kutoka serikalini na kuonesha kiasi cha shilingi bilioni 4.4 ikiwa ni sehemu ya ruzuku hiyo kama mapato yake kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Sikiliza pia:

Maoni: Vita visivyowezekana kupambana na ufisadi Tanzania